Header Ads

Ugonjwa wa Ini



Ugonjwa wa Ini

Ini ni kiungo muhimu sana katika mwili wa binadamu. Ndicho kiungo kikubwa kilichopo ndani ya mwili. Ugonjwa wa cirrhosis ni ugonjwa wa 12 duniani kati ya magonjwa yanayosababisha vifo vitokanavyo na  maradhi. Cirrhosis husababishwa na unywaji pombe kupindukia, ugonjwa wa hepatitis B, C, na ugonjwa wa fatty liver disease. Kwa wagonjwa wengine chanzo halisi cha ugonjwa huu hakijulikani. Kabla ya kuangalia ugonjwa wa cirhosis  (tamka sirosis kwa kiswahili), kwanza tuangalie kazi ya ini kwenye mwili wa binadamu.

Ini linahusika na

  • Kushughulikia chakula kilichosagwa kutoka kwenye utumbo mdogo (small intestine)
  • Hulinda mwili dhidhi ya magonjwa
  • Kutengeneza  nyongo (bile)
  • Hudhibiti kiwango cha mafuta, sukari na chembechembe zijulikanazo kama amino acids kwenye damu
  • Huhifadhi vitamini, madini ya chuma na kemikali nyengine muhimu
  • Huvunjavunja chakula na kutengeneza energy inayohitajika mwilini
  • Ini hutengeneza chembechembe zinazozuia damu kuganda mwilini kama fibrinogen, prothrombin, factor V, VII, IX, X  na X, protini C na S, antithrombin na nk.
  • Huharibu sumu na madawa ambayo yameingia mwilini.
  • Hutengeneza homoni aina ya angiotensinogen  ambayo inahusika kupandisha presha ya damu mwilini wakati inapokutana na enzyme ya renin, enzyme hii ya renin hutolewa na figo wakati figo inapohisi presha imeshuka mwilini.
  • Husafisha damu kutokana na chembechembe  mbaya na bakteria.
  • Hutengeneza enzyme na protini ambazo zinahitajika mwilini kwenye shughuli nyingi na hata kurekebisha tishu zilizoharibika.

Ugonjwa wa cirrhosis ni nini?

Cirrhosis ni matokeo ya ugonjwa sugu wa ini ambao  hubadilisha tishu za kawaida za ini kwa njia ya fibrosis, scar tishu, matezi (regenerative nodules),  kuziba damu kuingia kwenye ini  na hivyo kufanya ini kushindwa  kufanya kazi yake vizuri.

Visababishi vya ugonjwa huu

Cirhosis husababishwa na mjumuiko wa magonjwa mengi ambayo ni
Ugonjwa wa ini unaosababishwa na unywaji wa pombe kupindukia kwa muda mrefu ( alcoholic liver disease) . Inakadiriwa asilimia 10 – 20 ya wanywaji pombe kupindukia kwa miaka 10 au zaidi  ndio wanaopata ugonjwa huu. Yule anayekunywa pombe kwa muda mrefu huwa na asilimia kubwa ya kupata ugonjwa huu kutokana na kiwango cha pombe kuongezeka au kuwa kingi kwenye mwili wake. Pombe huharibu ini na kusababisha lishindwe kufanya kazi yake dhidhi ya mafuta, protini, na wanga (carbohydrates).
Ugonjwa huu wa ini unaotokana na unywaji pombe kwa muda mrefu (alcoholic liver disease) hauathiri wanywaji pombe wote na si lazima uwe mnywaji pombe ili upate ugonjwa huu.
Wanywaji pombe kupindukia pia wanaweza kupata tatizo la utapia mlo (malnutrition) kutokana na pombe kukosa virutubisho muhimu vinavyohitajika  mwilini, kupungua kwa hamu ya kula, na kupungua kwa ufyonzwaji wa virutubisho  vya chakula  kwenye utumbo. Utapia mlo pia husababisha ugonjwa wa ini.
Unywaji wa pombe kupindukia huweza kusababisha ugonjwa aina ya alcoholic hepatitis ambao huambatana na homa, manjano kwenye mboni au ndani ya macho na kwenye ngozi, kuongeza ukubwa wa ini (hepatomegaly) na kudhoofika  kwa mgonjwa (anorexia). Alcoholic hepatitis ni hatari sana kwani unaweza kusababisha kifo.
Non alcoholic steatohepatitis (NASH)  ama Non alcoholic liver cirrhosis   – Mafuta hujikusanya kwa wingi kwenye ini na kusababisha huharibifu wa tishu za ini (scar tishu). Ugonjwa huu unahusishwa na kisukari, unene uliopitiliza, utapia mlo wa protini (protein malnutrition), baadhi ya magonjwa ya moyo na baadhi ya madawa aina ya corticosteroids. Mgonjwa hapa hana historia ya unywaji pombe.
Ugonjwa aina ya hepatitis B, C, na D, ambayo husababishwa na virusi vya hepatitis. Hepatitis B ndio chanzo kikuu cha ugonjwa wa cirhosis kati ya hepatitis zote duniani. Hepatitis C ndio sababu kuu ya wagonjwa wengi kuhitaji ini la kupandikizwa (liver transplant) duniani.
  • Autoimmune hepatitis – Husababishwa na mfumo wa kinga mwilini ambao huathiri ini na kuharibu chembechembe au seli za ini na hivyo kusababisha ugonjwa wa cirrhosis.
  • Magonjwa ya kurithi kama cystic fibrosis, wilson’s  disease, galactosemia, alpha 1 antitrypsin deficiency, hemochromatosis na glycogen storage disease. Watu wenye tatizo la ukosaji wa alpha  - 1  -antitrypsin  ambayo inakuwa kwenye mapafu ya binadamu na husaidia kukinga tishu zisiharibiwe na enzyme za seli za uhabirifu hasa nuetrophil elastase, wanaweza kupata mjumuiko wa magonjwa yanayoathiri mfumo wa upumuaji  (COPD)  kama watakuwa na historia ya uvutaji sigara.
  • Cardiac  cirrhosis  - Hutokana na ugonjwa sugu wa moyo unaoathiri  sehemu ya kulia ya moyo na hivyo kuufanya moyo kushindwa kufanya kazi yake vizuri na hatimaye kulileletea madhara ini. Husababishwa na tatizo kwenye kizibo cha moyo (valve problem), kuathiriwa kwa moyo na maradhi ya bakteria au virusi, uvutaji sigara na nk.
  • Madawa na sumu  zinazoharibu na kudhuru ini
  • Ugonjwa wa kichocho (schistosomiasis)
  • Magonjwa yanayojulikana kama  primary biliary cirrhosis na primary  sclerosing  cholangitis

Dalili na viashiria vya ugonjwa wa cirrhosis

Wagonjwa wengi wa cirrhosis hawaonyeshi dalili zozote kwenye hatua za awali za ugonjwa huu. Dalili zinatokana na
  • Kushindwa kufanya kazi kwa ini kadri ugonjwa unavyoongezeka
  • Kuharibika kwa umbile na ukubwa wa ini kutokana na kitu tunachoita kitaalamu kama scarring

Dalili za cirrhosis ni

  • Uchovu
  • Ulegevu
  • Kichefuchefu
  • Kupungua hamu ya kula hatimaye kupungua uzito
  • Kupungua hamu ya kufanya mapenzi
Hata hivyo, dalili na viashiria vingi vinaweza visitokee hadi mtu atakapopata madhara ya cirrhosis. Dalili na viashiria hivyo ambavyo hutokea baada ya madhara kutokea ni kama zifuatavyo;
  • Kuwa rangi ya manjano kwenye macho na ngozi kutokana na ukusanywaji  wa bilirubin kwa wingi kwenye viungo hivi.
  • Kutapika
  • Homa
  • Kuharisha
  • Maumivu ya tumbo kutokana kuongezeka ukubwa wa ini au kutokana na vijiwe kwenye gall bladder (gallstones)
  • Kuwashwa mwili  kutokana na bile salts iliyopo kwenye ngozi
  • Tumbo kuwa kubwa au kuvimbiwa kutokana na maji kujikusanya sehemu ya tumbo (ascites)
  • Kuongezeka uzito kwa sababu ya ukusanywaji wa maji mwilini
  • Kutoka damu kwenye fizi au pua, husababishwa na kutokuwepo na chembechembe zinazozuia damu kuganda
  • Kuvimba kwa miguu
  • Kupumua kwa shida
  • Kupungua nyama mwilini (Loss of muscle mass)
  • Kwa wanawake, kuwa na hedhi isiyokuwa ya kawaida kutokana kupungua kwa utolewaji wa homoni zinazosaidia wakati wa hedhi.
  • Damu kwenye matapishi au haja kubwa kutokana kuharibika mfumo wa kuzuia damu kuganda.
  • Spider angiomata – Kutokea kwa mabaka yanayofanana na utandu wa buibui ambao katikati yake kuna rangi nyekundu. Hii inatokana na mishipa ya damu inayoonekana kwa sababu ya kuongezeka  kiwango cha estradiol.
  • Kuongezeka mikunjo ya kwenye viganja vya mikono (palmar erythema) husababishwa na kupungua kwa homoni za mapenzi (sex hormone)
  • Kuongezeka kwa matiti kwa wanaume (gynecomastia) kutokana na kuzidi kwa kiwango cha homoni aina ya estradiol mwilini, hutokea kwa asilimia 66 ya wagonjwa wa cirrhosis.
  • Kupungua kwa korodani  kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi vizuri kwa hypothalamus na pitituary gland. Hii husababisha uume kushindwa kusimama (kusimika),  kushindwa kutia mimba mwanamke (infertility), na kupungua hamu ya kufanya mapenzi.
  • Mabadiliko ya kucha – Kucha zinaweza kuwa na mistari (Muehrcke’s lines), au kuwa za rangi nyeupe pembezoni mwake na rangi nyekundu kwa mbele (terry’s nails) au kujikunja kwa kucha pembeni (finger clubbing).
  • Bandama kuongezeka ukubwa (splenomegaly)
  • Kuongezeka unene  na kufupika kwa ngozi ya viganja vya mikono na hivyo kusababisha vidole na viganja kuwa kwenye umbile la kujikunja (dupuytren’s contracture)
  • Ini linaweza kuongezeka ukubwa, kupungua au kuwa la kawaida.
  • Kuonekana kwa mishipa ya damu sehemu ya tumbo (caput medusa)
  • Mgonjwa kuwa na harufu kali kama ya maiti kwenye pumzi kutokana na kuongezeka kwa dimethyl sulfide
  • Cruveilhier   Bumgarten murmur – Sauti fulani ambayo daktari anaweza kuisikia  wakati akimpima mgonjwa kutumia stethoscope  maeneo ya tumboni.
  • Mapigo ya moyo kwenda haraka mtu anapojaribu kusimama
  • Kusikia kiu sana
  • Mdomo kuwa mkavu au kukauka mate
  • Asterixis
Caput medusa kama inavyoonekana

Vipimo vya uchunguzi

  • Vipimo vya damu (Complete blood count) – Upungufu wa damu (anaemia),  kupungua kwa chembechembe bapa  za damu au platelets (thrombocytopenia), kupungua chembechembe nyeupe za damu (leukopenia) na chembechembe aina ya neutrophils (neutropenia) na kupungua kwa madini aina ya sodium.
  • Kipimo cha ufanyaji kazi wa  ini (Liver function test) – Kupungua kwa albumin, kuongezeka kwa aminotraferases AST na ALT (AST > ALT), alkaline phosphatase, bilirubin, gamma glutamyl transferase. Kuongezeka kwa protini aina ya globulin.
  • Kipimo cha kuangalia chembechembe za kuzuia damu kuganda (coagulation test)
  • Liver biopsy
  • Vipimo vya damu kuangalia kiwango cha immunoglobulins (IgG, IgM, na IgA), Alpha 1 antitrypsin, ferritin na  transferrin saturation, copper na ceruloplasmin.
  • Serology for hepatitis virus, autoantibodies
  • Kipimo cha wingi wa mafuta aina ya cholestrol na sukari                                                                            
  • Vipimo vya mionzi
  • Kipimo cha ultrasound – Inaweza kugundua saratani ya ini, portal hypertension nk.
  • CT scan ya tumbo ili kutofautisha na magonjwa mengine kama saratani aina mbalimbali, magonjwa ya kongosho (pancrease), ini, figo nk.
  • Liver/bileduct MRI
  • Gastroscopy – Kipimo cha kuangalia mpira wa kupitishia chakula kwenda kwenye tumbo, tumbo na sehemu ya duedonum ili kuhakikisha kama kuna oesophagus varices na kuzitibu ikiwezekana.

Tiba ya ugonjwa wa cirrhosis inahusisha

  • Kuacha kunywa pombe kabisa kwa kupata ushauri nasaha pamoja na mgonjwa kuhudhuria programu za kusaidia kuacha kunywa pombe (rehabilitation center). Kama ugonjwa wa cirrhosis  bado haujatokea, mgonjwa akiacha pombe ini linaweza kupona.
  • Kutibu tatizo la utapia mlo kwa kutumia vitamini na folic acid.
  • Kutibu  chanzo cha ugonjwa wa  cirrhosis
  • Kuzuia uhabirifu zaidi wa ini kwa kuzuia utumiaji wa dawa aina ya paracetamol pamoja na pombe.
  • Chanjo dhidhi ya hepatitis B na C
  • Mgonjwa kupewa dawa za kuongeza damu na kama upungufu wa damu mwilini ni mkubwa basi atahitaji kupewa damu
  • Kuzuia madhara ya cirrhosis kwa
  • Kuzuia utumiaji wa chumvi kwenye chakula
  • Kupunguza vyakula venye protini nyingi
  • Kutumia dawa za antibiotics ambazo daktari atakushauri
  • Kutumia dawa aina ya lactulose ili kupunguza madhara ya heptic encephalopathy kwa kupunguza kiwango cha ammonia mwilini na pia husaidia mgonjwa kupata choo laini.

Madhara ya cirrhosis ni yapi?

Madhara ya cirrhosis ni kama yafuatayo
  • Saratani ya ini ambayo husababisha vifo vingi sana
  • Kuvimba kwa tumbo kwa sababu ya kujaa maji
  • Kuwashwa mwili mzima
  • Kuwa wa manjano kwenye macho na ngozi
  • Kudhurika rahisi na madawa
  • Kutoka damu kwenye fizi, puani na nk.
  • Kuongezeka kwa mifupa ya kwenye mikono na miguu na hivyo kusababisha maumivu makali sana, kukakamaa na kuvimba miguu.
  • Esophageal varices
  • Portal hypertension
  • Hepatic encephalopathy – Hali ya kuchanganyikiwa, kupungua kwa umakini, kusahau haraka, kuwa na hasira, kupungua uwezo wa kujiamulia, mgonjwa kutojali muonekano wake,  kubadilika badilika hisia, kuona watu au vitu ambavyo haviko (hallucination), matatizo ya kulala, hii inatokana na kuongezeka kwa ammonia ndani ya damu ambayo hupelekwa kwenye ubongo.
Madhara ya cirrhosis yakishindwa kudhibitiwa au kama ini litashindwa kufanya kazi kabisa, basi mgonjwa atahitaji kupandikizwa ini jingine.

No comments:

Powered by Blogger.